Sana’a. Mashambulizi ya angani yanayoshukiwa kufanywa na Marekani yamepiga maeneo yanayodhibitiwa na waasi wa Waouthi nchini Yemen hadi Jumatano, huku waasi hao wakidai kuwa mashambulizi hayo yamewauwa angalau watu sita kote nchini.
Wakati huo huo, picha za satelaiti zilizopigwa Jumatano na kuchambuliwa na shirika la habari la The Associated Press zinaonyesha kuwa kuna angalau mabomu sita ya siri ya B-2 Spirit sasa yamewekwa katika kisiwa cha Diego Garcia, kilicho katika Bahari ya Hindi hatua isiyo ya kawaida sana katikati ya kampeni ya kijeshi dhidi ya Wahouthi na mvutano na Iran.
Kampeni kali ya mashambulizi ya angani nchini Yemen chini ya Rais wa Marekani Donald Trump, ikilenga waasi hao kwa sababu ya mashambulizi yao dhidi ya meli katika maji ya Mashariki ya Kati yanayotokana na vita vya Israel na Hamas, imewauwa angalau watu 67, kulingana na takwimu zilizotolewa na Houthi.
Hakukuwa na dalili za kampeni hiyo kusitishwa, kwani utawala wa Trump uliendelea kuhusisha mashambulizi yake dhidi ya waasi wa Kihouthi wanaoungwa mkono na Iran na jitihada za kushinikiza Tehran kuhusu mpango wake wa nyuklia unaoendelea kwa kasi.
Ingawa Serikali ya Marekani haijatoa maelezo maalum kuhusu kampeni hiyo na malengo yake, msemaji wa Ikulu ya White House, Karoline Leavitt, alisema Jumanne kuwa mashambulizi yamefikia zaidi ya 200.
“Iran imepata pigo kubwa kutokana na mashambulizi haya, na tumeshuhudia viongozi wa Houthi wakipotezwa,” alisema Leavitt. “Tumewaondoa wanachama muhimu waliokuwa wakishambulia meli za kivita na meli za kibiashara, na operesheni hii haitaisha hadi uhuru wa usafiri wa baharini katika eneo hili urejeshwe.”
Wahuthi bado hawajakiri kupoteza kiongozi yeyote, na Marekani haijataja rasmi jina la kiongozi yeyote aliyelengwa. Hata hivyo, jumbe zilizovuja kutoka kwenye mawasiliano ya ‘Signal’ kati ya maafisa wa utawala wa Trump na kauli zao za hadharani zinaashiria kuwa kiongozi wa kikosi cha makombora cha waasi hao alikuwa miongoni mwa walengwa.
Hodeida yashambuliwa
Shambulio moja la angani linaloshukiwa kuwa la Marekani lililenga kile ambacho Houthi wamekiita “mradi wa maji” katika Wilaya ya Mansuriyah, mkoa wa Hodeida, na kusababisha vifo vya watu wanne huku wengine wakijeruhiwa.
Mashambulizi mengine yaliendelea hadi Jumatano, yakilenga mikoa ya Hajjah, Saada, na Sanaa, kulingana na waasi hao.
Hadi Jumatano usiku, Houthi walisema kuwa mashambulizi 17 yalipiga mkoa wa Saada, huku mtu mmoja akiuliwa katika shambulio kwenye bandari ya Ras Isa huko Hodeida na mwingine katika kituo cha mawasiliano kilichopo kwenye Mlima Jebel Namah, katika mkoa wa Ibb.
Waasi hao wanasema wameendelea kushambulia meli za kivita za Marekani katika Bahari Nyekundu, haswa meli ya kubeba ndege USS Harry S. Truman, ambayo ndiyo inayofanya mashambulizi mengi dhidi ya waasi hao.
Hakuna meli ya kivita ya Marekani iliyopigwa bado, lakini Jeshi la Wanamaji la Marekani limeeleza kuwa mashambulizi ya Houthi ni mapigano makali zaidi ambayo wanamaji wake wamekabiliana nayo tangu Vita Kuu ya Pili ya Dunia.
Meli nyingine ya kubeba ndege, USS Carl Vinson, ambayo kwa sasa iko Asia, iko njiani kuelekea Mashariki ya Kati kusaidia operesheni za USS Truman.
Mapema Jumatano, msemaji wa Pentagon, Sean Parnell, alisema kuwa “vikosi vya ziada na rasilimali nyingine za anga” vitapelekwa katika eneo hilo, lakini hakutoa maelezo zaidi.
Zaidi ya wanajeshi 300 wa anga na ndege kadhaa za kivita A-10 Thunderbolt II pia wamepelekwa Mashariki ya Kati kusaidia operesheni hiyo, wakiwa sehemu ya Kikosi cha Anga cha Taifa cha Idaho.
Wanajeshi hao, kutoka Kikosi cha 124 cha Kivita cha Idaho, wanaendesha ndege zinazojulikana kama Warthog.
Amri Kuu ya Kijeshi ya Marekani kwa Mashariki ya Kati (CENTCOM) ilichapisha picha Jumatano zikionyesha ndege mbili za A-10 zikifanya operesheni katika eneo hilo.
Mashambulizi makali
Uchunguzi wa shirika la habari la AP umebaini kuwa operesheni mpya ya Marekani dhidi ya Houthi chini ya Trump inaonekana kuwa kubwa zaidi kuliko zile zilizofanywa chini ya Rais wa zamani Joe Biden, huku Washington ikihamia kutoka kushambulia tu vituo vya kurushia makombora hadi kushambulia viongozi waandamizi wa waasi na kurusha mabomu katika miji.
Kampeni mpya ya mashambulizi ya angani ilianza baada ya waasi hao kutishia kuanza tena kushambulia meli zinazodaiwa kuwa za “Israel” kwa sababu ya Israel kuzuiya misaada kuingia Ukanda wa Gaza.
Waasi hao hawajatoa tafsiri wazi ya nini wanachokiita meli ya Israel, jambo ambalo linaweza kufanya meli nyingi kuwa malengo yao.
Tangu Novemba 2023 hadi Januari mwaka huu, waasi wa Houthi walishambulia zaidi ya meli 100 za kibiashara kwa makombora na droni, wakizamisha meli mbili na kuwauwa mabaharia wanne. Pia walijaribu kushambulia meli za kivita za Marekani, lakini bila mafanikio.
Mashambulizi haya yameongeza umaarufu wa waasi wa Houthi, ambao wanakabiliwa na matatizo ya kiuchumi na wameanzisha msako mkali dhidi ya wapinzani na wafanyakazi wa misaada nchini Yemen, huku vita vya miaka kumi vikiendelea kuliharibu taifa hilo maskini zaidi katika ulimwengu wa Kiarabu.